Katika blogu hii, tutachunguza njia mbalimbali za kuimarisha ufahamu wetu wa Biblia. Tutajadili mbinu za kusoma Biblia kwa ufanisi, vidokezo vya kukariri maandiko matakatifu, na mikakati ya kutumia somo la Biblia katika maisha yetu ya kila siku. Iwe wewe ni mtaalam wa Biblia mzoefu au unaanza tu safari yako ya imani, "Jifunze Biblia Zaidi" ni rasilimali kamili ya kukusaidia kuongeza ufahamu wako wa Maandiko Matakatifu na kumkaribia Mungu zaidi.

SHERIA YA JUMAPILI NA UNABII WA SIKU 2300, 1260, 1290, 1335 KATIKA DANIEL 8 NA 12 NA UFUNUO 13.

SHERIA YA JUMAPILI NA UNABII WA SIKU 2300, 1260, 1290, 1335 KATIKA DANIEL 8 NA 12 NA UFUNUO 13.



Ni unabii unaopaswa kujifunza kwa kina tukizingatia kwamba unalo fundisho kubwa kwetu sisi tunaoishi katika siku hizi za mwisho.

Nabii anasema: “Kuna ukweli mwingi muhimu katika Neno la Mungu, ‘Lakini ukweli wa leo’ ndio unahitajika kundini sasa. Niliona hatari ya wajumbe wanaoweka kando mada muhimu za ukweli wa leo na kukawia juu ya masomo ambayo hayalengi kuunganisha kundi na kutakasa moyo. Hapo Shetani atapata kila nafasi iwezekanayo ili kuharibu kazi ya Mungu.” {Maandiko ya Awali uk. 60}

 

Kwa bahati mbaya kabisa makundi mengi lilipo kanisa la Mungu (Masalio Watengenezaji wa kanisa la Waadventista Wa siku ya Saba –Sabato) wajumbe wa Mungu wamekuwa wakitilia mkazo masomo ambayo hayalengi kuunganisha kundi la Mungu na badala yake masomo hayo yanatenganisha zaidi na kusababisha mgawanyiko mkubwa ndani ya kanisa la Mungu. Upo ukweli wa leo ambao ukifundishwa katika uongozi wa Roho Mtakatifu, hitilafu na tofauti zinazoonekana katika kanisa la Mungu zitafutiliwa mbali na tutaona umoja na upendo ukitawala na kuwaweka watu tayari kwa kupokea mvua ya masika.

Lakini ukweli wa leo ni upi?  Nabii anaendelea kusema: “Lakini masomo kama hema takatifu pamoja na siku 2300, Amri za Mungu na imani ya Yesu, vinaeleza kwa usahihi mwamko uliopita wa wanamarejeo na kuonyesha msimamo wetu wa leo, kuimarisha imani ya mwenye mashaka na kuweka wazi utukufu ujao. Mara nyingi nilionyeshwa kuwa haya ndiyo masomo ya msingi ambayo wajumbe wa Mungu wanapaswa kukawia juu yake.” {E.G. White,Maandiko ya Awali uk. 60.}

 

Basi kwa sababu ya ushuhuda huu wa Mungu, kama tunahitaji kuwa na umoja na kutakaswa mioyo, hatuna budi kukawika juu ya masomo ya hema takatifu, unabii wa siku 2300 na Amri za Mungu na imani ya Yesu ambapo katika somo hili tutajikita zaidi kuhusu utimilifu wa unabii wa siku 2300.

 

“Nuru ile aliyoipokea Daniel kutoka kwa Mungu ilitolewa zaidi kwa ajili ya siku hizi za mwisho. Njozi alizoziona akiwa kwenye mto Ulai na Hiddekel, mito ile mikubwa ya Shinar, kwa sasa zipo kwenye mchakato wa utimilifu, na matukio yote yaliyoelezewa yatatimilika na kupita.” {E.G. White,TM 112. 3, 113.}

Njozi alizoona Danieli akiwa kwenye mto Ulai na Hidekkel ni njozi zinazohusu unabii wa siku 2300. Nabii anasema nuru hiyo ilitolewa zaidi kwa ajili ya siku hizi za mwisho na kwamba ‘kwa sasa njozi hizo zipo kwenye mchakato wa utimilifu, na matukio yote yaliyoelezewa yatatimia na kupita’, hii ikimaanisha kwamba ingawa unabii wa siku 2300 ulifikia mwisho mwaka 1844 kwa maana ya kutimia katika siku moja kwa mwaka, lakini matukio YOTE yaliyotimia kipindi hicho, yatatimia tena hadi mwisho wa wakati.

 

Siku 1260, 1290 na 1335 za unabii wa Danieli 12.

Unabii wa siku 2300 umetajwa katika mgawanyiko wa siku 1260, siku 1290 na siku 1335. Upo uhusiano mkubwa wa siku 1335 na watu 144,000 kwa sababu wale watakaofanikiwa kufika katika siku 1335 ndiyo watakaokuwa sehemu ya 144,000 na watajua kuwa ni sehemu ya 144,000 baada kipindi hiki kupita. Ufafanuzi wa hili utatolewa mbele ya fundisho hili.

Nabii anasema: “Ujumbe wa malaika wa kwanza na wa pili ulitangazwa, lakini pasingetolewa nuru zaidi hadi pale jumbe hizi zingekuwa zimefanya kazi yake iliyokusudiwa. Jambo hili linawakilishwa na malaika aliyesimama na kuweka mguu wake mmoja juu ya bahari akisema kwamba hapana wakati tena. Wakati huu unaotajwa na malaika kwa sauti kuu, siyo mwisho wa historia ya ulimwengu, wala siyo wakati wa kufungwa kwa mlango wa rehema, bali wa unabii wa siku moja kwa mwaka, ambao utatangulia marejeo ya Bwana wetu. Hii inamaanisha, watu hawatakuwa na ujumbe mwingine kuhusu wakati maalumu. Baada ya kupita kwa wakati huu, kufikia mwaka 1842 hadi 1844, hakutakuwepo na muda wa kufuatilia unabii wa nyakati (siku moja kwa mwaka). Ufuatiliaji mrefu kabisa unafikia mwaka 1844.” {E.G. White, SDA BC vol. 7 p. 971.}

 

Hii inamaanisha kwamba unabii huu utajirudia siyo katika utimilifu wa siku moja ya unabii sawa na mwaka mmoja halisi bali katika kujirudia kwa matukio. Hata hivyo hadi pale nuru ya ujumbe wa malaika wa kwanza na wa pili itakapofanya kazi ndani ya mioyo ya watu wa Mungu ndipo nuru zaidi itatolewa. Nuru inayotakiwa kufanya kazi mioyoni mwetu ili tupate nuru zaidi ni ujumbe wa kuhesabiwa haki kwa imani kwa maana ya kumruhusu Yesu akae na kutawala ndani yetu na kutegemea uongozi, msaada na ulinzi wake katika maisha yetu yote tukijua kwamba hatuwezi kutenda wema wowote kwa uwezo wetu isipokuwa kama Yesu anakaa ndani yetu. Je, umeuruhusu ujumbe wa malaika wa kwanza na wa pili kufanya kazi ndani yako ili Mungu akufunulie nuru zaidi ikiwa ni pamoja na unabii wa siku 2300? Hebu mruhusu Roho wa Mungu akusaidie katika kutimiza mapenzi ya Mungu kama ilivyo kwenye jumbe hizi za malaika wa kwanza na wa pili.
Unabii wa siku 2300 umegawanyika katika sehemu kuu mbili za utimilifu wake. Sehemu ya kwanza niutimilifu kuanzia mwaka 457KK hadi mwaka 1844BK na sehemu ya pili ni kuanzia mwaka 1844 hadi marejeo ya pili ya Bwana wetu Yesu Kristo.

1.     UTIMILIFU WA UNABII WA SIKU 2300 SEHEMU YA KWANZA.
Nini yalikuwa matukio katika kutimia kwa unabii wa siku 2300? “Ndipo nikamsikia mtakatifu mmoja akinena, na mtakatifu mwingine akamwuliza huyo aliyenena, Haya maono katika habari ya sadaka ya kutekezwa ya daima, na lile kosa lifanyalo ukiwa, yataendelea hata lini, kukanyagisha patakatifu na jeshi?” {Danieli 8:13.} Basi tukitafakari Andiko hili tunaona mambo makubwa mawili yaliyojenga msingi wa swali hili. Kwanza nisadaka ya daima ya kutekezwa na pili ni lile kosa lifanyalo ukiwa. Haya ndiyo matukio makubwa tunayohitaji kuyajifunza ili kupata kujua mantiki ya jibu lililotolewa katika swali hilo, yaani: “Hata nyakati za jioni na asubuhi elfu mbili na mia tatu; ndipo patakatifu patakapotakaswa.” {Daniel 8:14.} Jibu hili linatuonyesha pia kwamba upo uhisiano mkubwa kati ya siku 2300 na patakatifu (hema takatifu) lakini haya ni masomo mawili yanayotakiwa kujifunza kila moja kwa wakati wake.

Nabii Daniel anaendelea kutuambia kile alichoambiwa na mtakatifu katika habari ya siku 2300, anasema: “Muda wa majuma sabini umeamuriwa juu ya watu wako, na juu ya mji wako mtakatifu ili kukomesha makosa, na kuishiliza dhambi, na kufanya upatanisho kwa ajili ya uovu, na kuleta haki ya milele, na kutia muhuri maono na ubaii, na kumtia mafuta yeye aliye Mtakatifu. Naye atafanya agano thabiti na watu wengi kwa muda wa juma moja; na kwa nusu ya juma hiyo ataikomesha sadaka na dhabihu; na mahali pake litasimama chukizo la uharibifu; na hivyo hata ukomo, na ghadhabu iliyokusudiwa imemwagwa juu yake mwenye kuharibu.” {Daniel9:24; 27}

Waisraeli walipewa muda wa majuma 70 ili wajitakase na kuacha dhambi na kwamba kipindi hicho kilikuwa ni kipindi cha rehema kwao ambapo baada ya muda huo kupita, mlango wa rehema kwao ungekuwa umefungwa.Unabii wa siku 2300 ulianza kutimia mwaka 457KK na hapa ndio mwanzo wa majuma sabini. Majuma 70 ni sawa na siku 490 na katika unabii wa siku moja kwa mwaka mmoja, hii ni miaka 490. Ukichukua miaka 490 na kutoa miaka 457 jibu ni miaka 33 ambapo Masihi alikatiliwa mbali (alikufa juu ya mti wa mateso). Maandiko yanatuambia kwamba wakati huo mlango wa rehema kwa taifa la Israeli ulifungwa rasmi. Hivyo kipindi cha majuma 70 sawa na miaka 490 kilikuwa ni kipindi cha rehema kwa taifa la Israeli.
Katika Matthayo 18:22 Yesu alisema: “……Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini.” Je, Yesu alimaanisha mwisho wa kusamehe ni 7x70 = 490 au alimaanisha nini? Hapa Yesu alikuwa na maana ya kiroho zaidi na siyo katika mtazamo wa hesabu. Ieleweke kwamba Mungu hufanya kazi katika namba na kwamba namba anazotumia ni 1 hadi 12 na kila namba ina maana yake ya kiroho. Namba 490 katika maana ya kiroho humaanisha kipindi cha rehema kabla ya kufungwa kwa rehema. Kwa vile Waisraeli walipewa muda wa majuma 70 yaani 7x70 = 490 kama kipindi cha rehema, Yesu alimaanisha pia kuwa tunapaswa kusamehe siku zote hadi wakati mlango wa rehema utakapofungwa. Kwa ufupi matukio makubwa tunayoyapata ndani ya majuma 70 ni kusulubishwa kwa Yesu na kufungwa kwa mlango wa rehema kwa taifa la Israeli. Nini kilitokea baada ya mlango wa rehema kufungwa kwa taifa la Israeli? Walichaguliwa wamataifa ili kushika nafasi ya Israeli ya zamani. Zingatia: Hitimisho hili lina maana kubwa katika kurudiwa kwa utimilifu wa unabii huu siku za mwisho.

Siku 1260, 1290 naChukizo la Uharibifu
Baada ya kuangalia matukio ya kusulubishwa kwa Yesu yaani ‘kukomesha Sadaka ya daima ya kutekezwa’, pamoja na kufungwa kwa mlango wa rehema kwa taifa la Israeli, yaani ‘muda wa majuma 70 umeamuliwa juu ya watu wako’ sasa tuangalie tukio la ‘Chukizo la uharibifu.’ Nabii Daniel anasema: “Na tangu wakati ule ambapo sadaka ya kutekezwa ya daima itaondolewa, na hilo chukizo la uharibifu litakaposimamishwa, itapita siku elfu na mia mbili na tisini.” {Daniel 12:11.}
Kuondoa sadaka ya daima ya kuteketezwa inamaanisha kukomesha sheria za kusamehewa dhambi kwa njia ya kutoa kafara za wanyama na kuziteketeza juu ya madhabahu ya kutolea kafara. Je, ni kwa njia gani mwanadamu angesamehewa dhambi baada ya kuondoa sheria za kutoa kafara kwa ajili ya ondoleo la dhambi? Ni nani mwenye haki ya kusamehe dhambi? Imeandikwa: “Naye YESU alipoiona imani yao, akamwambia yule mwenye kupooza, Mwanangu, umesamehewa dhambi zako. Na baadhi ya waandishi walikuwa huko, wameketi wakifikiri mioyoni mwao, Mbona huyu anasema hivi?, anakufuru. Ni nani awezaye kusamehe dhambi isipokuwa mmoja, ndiye Mungu?” {Marko 2:5,6}
Nabii anasema tukio la kuondoa sadaka ya kuteketezwa ya daima lilifuatiwa na‘kusimamishwa kwa chukizo la uharibifu.’Je, ni wakati gani ambapo chukizo la uharibifu’ lilisimamishwa kwa mara ya kwanza? Ni wakati ule ambapo kanisa lilidhamiria kuwa na mamlaka ya kiserikali na kidini na kwamba kiongozi wa kanisa (Papa) na maaskofu na mapadri wa kanisa ndiyo wenye mamlaka na haki ya kusamehe dhambi kwa kutumia kimakosa kauli ya Yesu aliposema: “Amini nawaambieni, yoyote mtakayoyafunga duniani yatakuwa yamefungwa mbinguni; na yoyote mtakayoyafungua duniani yatakuwa yamefunguliwa mbingu.” Matthayo 18:18.
Je, hayo yalitendekea lini? Mwaka 508BK. Hivyo kwa kusema:“Na tangu wakati ule ambapo sadaka ya kutekezwa ya daima itaondolewa, na hilo chukizo la uharibifu litakaposimamishwa, itapita siku elfu na mia mbili na tisini” unabii huu ulimaanisha baada ya siku 1290 kutakuwa na tukio jingine muhimu katika mfululizo wa matukio ya utimilifu wa unabii wa siku 2300. Kwa ufupi tunaweza kusema kwambamwanzo wa siku 1290 ni mwaka 508BK wakati wa kutumizwa kwa tukio la chukizo la uharibifu (mamlaka ya kusamehe dhambi kuwekwa mikononi mwa wanadamu)baada ya sadaka ya kutekezwa ya daima kuondolewa mwaka 33 kwa kafara ya Yesu kutimiliza sheria ya kafara za wanyama. Ni tukio gani lilifuata mwishoni mwa siku 1290? Mwisho wa siku 1290 ni mwaka 1798 na tukio lililotimilizwa mwaka huo ni ‘kimoja cha vichwa vya mnyama kupatwa na jeraha la mauti’.
Lakini pia tunatambua kwamba mateso dhidi ya watu wa Mungu yalianza rasmi mwaka 538 na kudumu kwa miaka 1260. Kuna tofauti ya siku 30 kati ya siku 1290 na siku 1260. Hii inamaanisha kwamba kulikuwa na kipindi cha miaka 30 kwa watu wa Mungu kujiandaa kwa ajili ya mateso kutokana na kutokuamini juu ya msamaha wa dhambi uliotolewa na wanadamu. Tutaona pia kwamba wakati unabii huu unajirudia katika siku za mwisho kutakuwa na kipindi cha kujiandaa kwa watu wa Mungu tangu siku ya tangazo la sheria ya jumapili hadi wakati wa ulazimishwaji na kuwekwa sheria ya kutokuuza wala kununua kwa wale watakaokataa kutii sheria ya kuitunza sabato bandia ya siku ya kwanza ya juma tofauti na Sabato halisi ya siku ya saba.

Uheri wa kuzifikia siku 1335
“Heri angojaye, na kuzifikilia siku hizo elfu na mia tatu na thelathini na tano.” {Daniel 12:12.}
Je, siku 1335 zilianza lini? Katika Daniel 12:11 tunapewa mwanzo wa siku 1290 ikiwa ni sawa na mwanzo wa siku 1335 kwa sababu mstari wa 12 ni muendelezo wa kile kilichoanza kuelezewa kwenye mstari wa 11. Ukichukua mwaka 508BK na kujumlisha siku sawa na miaka 1335 utapata mwaka 1843. Maandiko yanatuambia kwamba William Miller alianza kuhubiri ujumbe wa utimilifu wa unabii wa siku 2300 mwaka 1843. Kwa nini HERI YULE ANGOJAYE na kuzifikia siku 1335? Kuna sababu kubwa mbili za uheri huu. Sababu ya kwanza ni kwamba mwisho wa siku 1335 ulikuwa ni wakati wa kuanza rasmi kuhubiri ujumbe wa malaika watatu katika utimilifu wa siku 2300 na kutakaswa kwa patakatifu. Ulikuwani wakati wa malaika wasaba kupiga baragumu yake. Nabii Yohana anasema: “isipokuwa katika siku za sauti ya malaika wa saba atakapokuwa tayari kupiga baragumu; hapo ndipo siri ya Mungu itakapotimizwa; kama alivyowaambia watumishi wake hao manabii.” {Ufunuo 10:7.}Kwa miaka mingi Sabato ilikuwa imetupiliwa mbali, mashahidi wawili (Neno la Mungu katika agano la kale na agano jipya) walikuwa wameuawa wakati wa mapinduzi ya Ufaransa kwa kuichoma moto Biblia na kuzuia watu kusoma Neno la Mungu. Lakini Mungu alikusudia kwamba mwisho wa siku 1335, siri yake iliyokuwa imetiwa muhuri katika unabii wa siku 2300 sasa ifunuliwe kwa ulimwengu na watu wake wajue huduma inayofanywa na kuhani wao Mkuu katika patakatifu pa mbinguni. Yule aliyengoja kwa uvumilivu aliitwa mwenye heri maana alipata nafasi ya kushuhudia siri ya Mungu ikifunuliwa. Sababu ya pili ya uheri ni kwamba wakati huo ulikuwa ni wakati wa kufungwa kwa mlango wa rehema kwa watumishi walioitwa shambani mwa Bwana mnamo saa 6 (Matthayo 22:1-14). Maandiko yanasema ujumbe wa malaika wa pili uliotangaza anguko la Babeli ulihubiriwa mwaka 1844 na kwamba wale waliokataa kutii ujumbe wa kutoka Babeli kama mfumo wa kanisa, mlango wa rehema kwao ulifungwa. Waprotestant waliokuwa waaminifu katika kupinga mafundisho ya kanisa la Rumi lakini wakakataa nuru ya Sabato, kwao mlango wa rehema ulifungwa mwaka 1844 na ilipofika saa 9 Mungu akawaita Waadventisa wa Sabato kuchukua nafasi yao.Katika kuwaita watumwa wake, Yesu alisema watumwa wa kwanza waliitwa ‘alfajiri’ ikiwakilisha kuitwa kwa taifa la Israeli kama taifa teule la Mungu. Hata hivyo wahakuwa waaminifu na ilipofika saa 3, mitume waliitwa kuchukua nafasi hiyo. Lakini pia mitume waliuacha upendo wao wa kwanza na kuruhusu Upapa kuinuka ambapo ilipofika saa 6 Waprotestant waliitwa ili kupinga madanganyo ya kanisa la Rumi. Kwa sababu ya kukataa ujumbe wa malaika wa kwanza na wa pili, tangazo la anguko kwa Waprotestant lilitolewa mwaka 1844 na ilipofika saa 9 Waadventista wa Sabato (SDA) waliitwa. WaSDA walifanya kazi kwa uaminifu kwa muda wa chini ya saa mbili maana ilipofika saa 11, watumishi wengine waliitwa ili watoke ndani ya kanisa asi la SDA wakiwa ni masalio waaminifu wazishikao amri za Mungu na imani ya Yesu.
Mpaka hapa tumeona kwamba mwisho wa majuma 70 ulikuwa ni mwisho wa rehema kwa taifa la kiyahudi kuitwa kama watu wa Mungu. Wayahudi walifungiwa mlango wa rehema baada ya mumkataa Yesu kama Masihi. Tumeona pia kwamba mwisho wa siku 1335 ulikuwa ni wakati wa kufungwa kwa rehema kwa mfumo wa Uprotestant kama taifa la Mungu na hili lilitokea baada ya Uprotestant kuikataa Sabato kama siku iliyowekwa na Mungu kwa ajili ya kumuabudu. Lakini yule aliyengoja akimtumaini Yesu alikuwa na heri maana huyo ndiye aliyefunuliwa nuru ya Sabato na kukubali kuhama na Kristo kutoka chumba cha pili cha patakatifu na kuingia naye kwa imani katika chumba cha pili cha patakatifu pa patakatifu kwenye hema iliyoko mbinguni isiyotengenezwa kwa mikono ya mwanadamu.

Lakini nini kilitokea wakati unabii wa siku 2300 unaendelea kutimia? Lipo tukio jingine muhimu ambalo limewekwa kwetu kama fundisho kuu. Tukio hili niangamizo la Yerusalemu lililotokea mwaka 70.

2.     Angamizo la Yerusalemu mwaka 66na70 na kukimbilia milimani.
Nabii Ellen White aliandika akisema kwamba kipindi cha mwaka 27 hadi 70 katika taifa la Israeli kilikuwa ni kipindi kinachofananishwa na angamizo la ulimwengu wote lakini uangamivu huu utaanzia katika Hekalu na nyumba ya Mungu, Ezekieli 9:6. Hakuna shaka kwamba historia ya Wayahudi kuanzia mwaka 27 hadi 70 ilikuwa ni utimilifu wa kujirudia kwa unabii wa Ezekieli 9.
Sura ya kwanza ya kitabu cha Pambano kuu inaelezea kile kitakachotokea katika siku za mwisho. Angamizo hili litaanza katika nyumba ya Mungu, yaani kanisa asi la SDA ambalo Mungu alilipatia upendeleo wa nuru kubwa katika nyumba ya Yakobo. {5T 211; Ezekieli 9:6}
“Wakati ujio wa majeshi ya Rumi ulikuwa ni ishara kwa wanafunzi juu ya angamizo la Yerusalemu, hivi ndivyo ilivyo kwamba uasi huu [sheria ya jumapili] ni ishara kwetu ya kufikia ukomo wa uvumilivu wa Mungu, kwamba kipimo cha uovu wa taifa letu [Marekani] kimejaa, na kwamba malaika wa rehema amekaribia kupaa na kamwe asirudi tena. Kisha watu wa Mungu watapitia katika kipindi kigumu na mateso ambayo nabii ameyaelezea kama taabu ya Yakobo. Kilio cha waaminifu na wanaoteswa kitafika mbinguni. Na kama damu ya Habili ilivyotoa kilio kutoa ardhini, sauti pia zinazotoa kilio kwa Mungu kutoka kwenye makaburi ya wafia dini, kutoka kwenye maiti zilizomo baharini, kutoka kwenye mapango ya milimani: ‘mpaka lini Bwana, Mtakatifu na wa kweli, hutahukumu na kulipa kisasi cha damu yetu kwa wale wakaao katika nchi’”? {5T 451.2}
“Sasa siyo wakati kwa watu wa Mungu kudumisha mapenzi yao au kuweka hazina zao katika ulimwengu. Muda si mwingi wakati, kama ilivyokuwa kwa wanafunzi wa awali, tutalazimishwa kutafuta makao kwenye maeneo yasiyokaliwa na watu. Kama ilivyokuwa kuzungukwa kwa Yerusalemu na majeshi ya Rumi kuwa ishara kwa wakristo wa Judea, kujipatia mamlaka kwa taifa letu katika kutangaza sabato ya Papa itakuwa ni onyo kwetu. Utakuwa ni wakati wa kuondoka kwenye miji mikubwa, maandalizi ya kuondoka kwenye miji midogo tayari kukimbilia milimani. Na sasa badala ya kutafuta makazi ya thamani kubwa hapa, tunapaswa kujiandaa kuondoka na kwenda kwenye nchi nzuri ya mbinguni. Badala ya kutumia mali zetu katika kujifurahisha, tunapaswa kujifunza jinsi ya kubana matumizi.” {5T 464-5}

Angamizo la Yerusalemu ni kielelezo cha kile kitakachotokea wakati wa kutangazwa kwa sheria ya jumapili. Wakati majeshi ya Rumi yalipouzunguka mji wa Yerusalemu mwaka 66 ilikuwa ni dalili na muda wa kuanza kuondoka mjini Yerusalemu na kukimbilia kwenye milima ya Pella, tangazo la sheria ya jumapili itakuwa ni ishara ya kuanza kuondoka kwenye miji mikubwa na kukimbilia kwenye miji midogo tayari kwa kukimbilia milimani. Ni wazi kwamba hatutakimbilia milimani wakati tangazo la sheria ya Jumapili litakapotolewa. Mwanzoni hakutakuwa na ulazimishwaji wa kuitunza Jumapili wala adhabu kwa wale wasioitii sheria ya jumapili. Kama sheria hii ingeanza moja kwa moja na kutokuruhusu kuuza na kununua, kufungwa gerezani na kukabiliwa na kifo, basi tusingepata muda wa kufanya maandalizi ya kukimbilia milimani.Kadri hukumu za Mungu zitakavyozidi kuwa kubwa kwa sababu ya kutangaza sabato bandia kinyume na Sabato ya kweli, sababu za hukumu hizi zitapelekwa kwa wale wasiokubali kuitunza sheria ya jumapili.

3.     UTIMILIFU WA UNABII WA SIKU 2300 SEHEMU YA PILI.
Katika unabii wa siku 2300 sehemu ya kwanza tumeona matukio yaliyotukia katika siku 1260 na 1290. Wakati unabii huu unatimia kwa mara ya kwanza tuliona kwamba siku 1290 zilihusika kwa tukio la kukomesha sadaka ya kuteketezwa ya daima na mahli pake kusimamisha chukizo la uharibifu, ambapo unabii huu unapojirudia kwa mara ya pili tukio hili litakuwa sawa na tangazo la kukomesha ibada ya siku ya Saba, Sabato ya Mungu na mahali pake kuwekwasheria ya jumapili, yaani, chukizo la uharibifu. Wakati wa utimilifu wa unabii huu sehemu ya kwanza, kulikuwa na kipindi cha siku 30 za maandalizi kwa ajili ya mateso yaliyoanza katika siku ya kwanza ya siku 1260. Wakati wa kurudiwa kwa utimilifu wa unabii huu siku za mwisho tunajifunza kwamba kutakuwa na kipindi cha kufanya maandali ya dhati mara baada ya tangazo la sheria ya jumapili kutolewa. Watu wa Mungu watakuwa wakijiandaa kwa mateso makali ambayo hayajawahi kutokea tangu kuumbwa kwa msingi wa dunia. Baada ya kipindi hiki kupita, jeraha la mauti litakuwa limepona katika utimilifu wake na ndipo tutashuhudia mnyama akishika tena mamlaka aliyoyapoteza mwaka 1798. Kipindi hiki ni sawa na kipindi kilichosemwa na nabii Yohana katika Ufunuo 13:1-5 cha utawala wa mnyama kwa muda wa miezi 42 au miaka mitatu na nusu.
Lakini pia ipo tofauti ya siku 75 kati ya siku 1335 na siku 1260 ambapo tofauti ya kipindi hiki inawakilisha kipindi cha kujiandaa kukimbilia milimani pamoja na kipindi cha kukaa milimani. Tumeona kipindi cha maandalizi kikiwakilishwa na siku 30 tangu kutolewa kwa sadaka ya kuteketezwa ya daima na kusimamishwa kwa chukizo la uharibifu na unapochukua 75 – 30 = 45 ambapo kipindi cha siku 45 kinawakilisha kipindi cha kukaa milimani kumsubiri Bwana na Mwokozi wetu. Hii ndiyo sababu ya uheri kwa wale watakaozifikia siku 1335 kwa sababu watakutwa na Yesu wakiwa hai, yaani wale 144,000. Wakati wa angamizo la Yerusalemu wale waliokimbilia milimani waliponya nafsi zao kama ilivyokuwa kwa Lutu ambaye pia aliponya nafsi yake baada ya kutoka Sodoma na kukimbilia kwenye mapango. Nimeelezea zaidi kuhusu 144,000 kwenye somo jingine.

Chukizo la Uharibifu na Kosa liletalo ukiwa.
“Ndipo nikamsikia mtakatifu mmoja akinena, na mtakatifu mwingine akamwuliza huyo aliyenena, Haya maono katika habari ya sadaka ya kutekezwa ya daima, na lile kosa lifanyalo ukiwa, yataendelea hata lini, kukanyagisha patakatifu na jeshi?”Daniel 8:13
“Na tangu wakati ule ambapo sadaka ya kutekezwa ya daima itaondolewa, na hilo chukizo la uharibifulitakaposimamishwa, itapita siku elfu na mia mbili na tisini.” {Daniel 12:11.}
Kusimamishwa kwa chukizo la uharibifu kulikosemwa na Daniel katika sura ya 12:11 ni tofauti na lile kosa liletalo ukiwa katika sura ya 8:13. Wakati chukizo la uharibifu linasimamishwa na nguvu kutoka nje ya watu wa Mungu kama tulivyoona, kwa upande mwingine lile kosa liletalo ukiwa linasababishwa na watu wa Mungu ndani ya hekalu au nyumba ya Mungu. Tumeona kwamba katika utimilifu wa unabii wa siku 2300 sehemu ya kwanza chukizo la uharibifu lilisimamishwa na nguvu ya kanisa la Rumi kwa kudai kuwa na mamlaka ya kusamehe dhambi. Lakini pia katika Ezekiel 8:9-18 tunaambiwa habari ya machukizo yaliyokuwa yanafanyika ndani ya hekalu la Mungu chini ya uongozi wa wazee (viongozi wa kanisa). Tumeona kwamba katika siku za mwisho chukizo la uharibifu linamaanisha kusimamishwa kwa sheria ya jumapili.Na sasa swali linaulizwa, nini maana ya ‘lile kosa lifanyalo ukiwa?’ Jibu ni kwamba ‘lile kosa lifanyalo ukiwa’ inamaanisha viongozi wa kanisa asi la SDA watawalazimisha washiriki wao kuitunza siku ya Jumapili. Je, hili litatokea? NDIYO.
Nabii anasema: “Bwana na vita na watu wanaodai kuwa Wake katika siku hizi za mwisho. Katika vita hii watu walioshika nyazifa za juu watachukua masimamo kinyume na msimamo aliouchukua Nehemia. Siyo tu kwamba hawataijali Sabato, bali pia watajaribu kuitunza kwa kuizika chini ya takataka za desturi na mapokeo. Katika makanisa na katika mikusanyiko ya wazi, watendakazi watawaeleza watu umuhimu wa kuitunza siku ya kwanza ya juma. Kuna majanga kwenye bahari na nchi kavu: na majanga haya yataongezeka, janga moja likifuatiwa na jingine; na kundi dogo la watunza Sabato litasondwa kidole kama linalosababisha uwepo wa ghadhabu ya Mungu juu ya ulimwengu kwa sababu hawaijali Jumapili.” {E.G White, R&H 18-3-1884.} Ukweli ni kwamba viongozi wa kanisa asi la SDA wataungana na adui katika kusimamisha chukizo la uharibifu (sheria ya jumapili) katika kurudia kwa utimilifu wa unabii wa siku 2300 ikiwa ni mwanzo wa siku 1260 baada ya jeraha la mauti kupona kwa ukamilifu wake. Jeraha la mauti halitapona kikamilifu mwanzoni mwa siku 1290 wakati wa tangazo la sheria ya jumapili. Kwa nini ninasema hivyo? Kwa sababu Daniel 12:11 anasema kwamba chukizo la uharibifu (kupona kwa jeraha la Kanisa la Rumi na tangazo la sheria ya jumapili) litasimamishwa siku ya kwanza katika siku 1290 ikiwa ni badiliko la kisheria la kuondoa Sabato ya kweli na kusimamisha sabato bandia ikifuatiwa na kutolewa kwa adhabu, mateso na kifo katika siku ya kwanza ya siku 1260. Hivyo ‘lile kose lifanyalo ukiwa’ linafanyika ndani ya kanisa asi la SDA kwa kuungana na mnyama kushinikiza utunzaji wa siku ya kwanza ya juma. Kwa jinsi gani kutakuwepo na ‘ukiwa’?  Ni kwa sababu Mungu atakuwa ameliacha kanisa na kushikamana na uzao wa mwanamke (kanisa) hao waliosali, wazishikao amri za Mungu na imani ya Yesu (Tazama Ufunuo 12:17). Itakumbukwa kwamba wakati Yesu alipowaacha wayahudi na hekalu lao aliwaambia: “Angalieni, nyumba yenu imeachwa hali ya ukiwa.” {Matthayo 23:38}

Kwa nini kurudiwa kwa unabii wa siku 2300 ni Muhimu?
Tunatambua kwamba unabii wa siku 2300 ulifikia mwisho mwaka 1844. Je, unabii huu ulitolewa kwa jinsi gani? Nabii Daniel anasema: “Ndipo nikamsikia mtakatifu mmoja akinena, na mtakatifu mwingine akamwuliza huyo aliyenena, Haya maono katika habari ya sadaka ya kutekezwa ya daima, na lile kosa lifanyalo ukiwa, yataendelea hata lini, kukanyagisha patakatifu na jeshi?” {Danieli 8:13.}Majibu yakatolewa: “Hata nyakati za jioni na asubuhi elfu mbili na mia tatu; ndipo patakatifu patakapotakaswa.” {Daniel 8:14.}
Hivyo tunatambua kwamba siku 2300 zilikuwa ni kipindi cha kukanyagisha patakatifu na jeshi. Lakini kwa nini unabii huu uliendelea hadi mwaka 1844 wakati Papa alikamatwa mateka na kufa nchini Ufaransa mwaka 1798? Je, miaka 46 ilikuwa miaka ya nini wakati kukanyagisha patakatifu na jeshi kuliishia mwaka 1798? Ninakubaliana na sehemu ya utimilifu wa unabii wa siku 2300 lakini tunaona kwamba unabii huu haukutimia kwa ukamilifu wake. Je utimilifu wake kikamilifu ni wa jinsi gani? Mfalme Justinian alikabidhi mamlaka kwa Papa ambapo Papa alikaa karibia miaka minne kabla ya kutumia madaraka yake aliyokabidhiwa ili kukanyagisha patakatifu na jeshi. Kwa ilikuwepo miaka kadhaa iliyojumuishwa katika muda ulio ndani kati yam waka 1798 na 1844.Mwaka 66 BK Warumi walikanyaga ardhi ya wayahudi lakini hawakufanya mashambulizi yoyote wakati huo. Amiri jeshi wa Rumi, Celstius aliondoa majeshi yake na kurudi Roma. Kipindi hiki kilitabiriwa katika unabii kama kipindi cha wayahudi kuondoka Yerusalemu na kukimbia kwenye milima ya Pella. Walikimbia nje ya Yerusalemu miaka mitatu na nusu kabla ya uvamizi wa jeshi la Rumi mwaka 70. Miaka hii mitatu na nusu inawakilisha kipindi ambapo unabii huu unapojirudia watu wa Mungu watatakiwa kukimbia kutoka miji mikubwa na kufanya maandalizi ya kukimbilia milimani. Nabii Ellen White ameelezea kwa kina katika sura ya kwanza ya kitabu cha Pambano kuu. Wapo wanaofanya makosa wakisema kwamba wakati tangazo la sheria ya jumapili linatolewa, itakuwa ni kipindi cha kutoka ndani ya kanisa asi la SDA na makanisa mengine. Hili ni kosa kubwa maana wakisubiri kipindi hicho watakuwa wamechelewa kuokoa nafsi zao kwa sababu hukumu za Mungu zitaanza ndani ya kanisa lake kwa watu waliopewa upendeleo mkubwa wa nuru hivyo watapimwa katika mizani ya hekalu sawasawa na wingi wa nuru waliyopewa [Tazama 5T 211].
Sasa tunaweza kufupisha kama ifuatavyo:

1.     Sheria ya jumapili itatangazwa. Hakuna adhabu yoyote mwanzoni mwa tanganzo la sheria hii. Tangazo litatolewa siku ya kwanza ya siku 1290 katika kujirudia kwa matukio ya unabii wa siku 2300. Katika siku ya kwanza ya siku 1260 ndipo sheria ya kutokununua wala kuuza sambamba na adhabu za mateso, vifungo na kifo zitatolewa.
2.     Tofauti ya siku 30 kati ya siku 1290 na siku 1260 zinawakilisha kipindi cha kukimbia kutoka miji mikubwa na maandalizi ya kuhama kwenda milimani tangu tangazo la sheria ya jumapili kutokewa na kabla ya kuanza kwa mateso.
3.     Katika siku ya kwanza ya siku 1260, hukumu za Mungu zinaanza kwa sababu ya kupuuza sheria Yake. Hukumu zitaongezeka zaidi na watakatifu watalaumiwa kuwa wanasababisha hukumu hizo kwa sababu wamekataa kutii jumapili.
4.     Ellen White anafananisha sheria ya jumapili na ujio wa kwanza wa jeshi la Rumi katika ardhi ya wayahudi mwaka 66. Kipindi hiki kitakuwa ni kwa ajili ya kuondoka kwenye miji mikubwa na kukimbilia kwenye midogo kwa maandalizi ya kukimbilia milimani {Tazama 5T 464-5}
5.     Tunatambua kwamba kutakuwa na kipindi kinachowakilishwa na miezi 42 ya mateso baada ya jeraha la mauti kupona kimamilifu (Ufunuo 13:1-5). Wakati wa tangazo la sheria ya jumapili jeraha la mauti litakuwa limepona lakini siyo kikamilifu.
6.     Kipo kipindi cha ‘kukanyagisha patakatifu na jeshi’ kitakachotumiwa na viongozi wa kanisa asi la SDA kwa kuwalazimisha waumini wao kuitunza jumapili. Kipindi hiki kitaendelea hadi wakati wa kufungwa kwa mlango wa rehema baada ya patakatifu kutakaswa ambapo kujirudia kwa unabii wa Ezekiel 9 kutasababisha angamizo la kanisa asi ya SDA na mchakato wake mpya. Mapigo saba hayatamwagwa juu ya dunia hadi mlango wa rehema utakapofungwa.

Kutakuwepo na matangazo mawili. Tangazo la kwanza litatolewa siku ya kwanza ya siku 1290 na kutakuwepo na siku 30 za maandalizi ya watu wa Mungu kukimbilia milimani na siku ya kwanza ya siku 1260 litakuwa ni tangazo la kifo kwa wale watakaokaidi kuitunza jumapili. Tangazo la pili litatolewa baada ya kufungwa kwa mlango wa rehema na mapigo saba yataanza kumwangwa juu ya nchi. Nabii Ellen White anasema hakutakuwepo na wafia dini baada ya kufungwa kwa mlango wa rehema lakini kutatolewa tangazo la kifo kutaka kujaribu kuwaua wale 144,000 ambapo silaha za adui zitakuwa kama manyasi hivyo tangazo hilo halitapata mafanikio. Kwa hiyo tangazo moja la kifo linafanikiwa kusababisha vifo vya wafia dini waaminifu na tangazo la pili halifanikiwi kwa sababu mlango wa rehema utakuwa umefungwa duniani kote na wale waaminifu watakuwa hai wasionje kifo kama Henoko na Eliya walivyopaa mbinguni bila kuonja mauti.
‘Lile kosa liletalo ukiwa’ linalosababishwa na kanisa asi la SDA linaufanya unabii wa siku 2300 kuwa na umuhimu mkubwa wa kujirudia. Kisha kutakaswa kwa mwisho kwa patakatifu pa Mungu kutafanyika ikiwa siyo mwanzo wa kutakaswa kwa patakatifu kama ilivyokuwa katika historia ya utimilifu wa unabii huu uliofikiwa mwisho wake mwaka 1844.
Wale wanaongejea na kuzifikilia siku 1335 wana heri kwa sababu wanajua kwamba kama watakimbilia milimani, watakuwa salama. Wale wote wanaokimbilia milimani wataletwa katia agano na Mungu kama ilivyoandikwa na nabii Ezekieli 20:34-38. Wataendelea kutoa kilio kikuu wakiwa jangwani ambao wale waliopokea alama ya mnyama bila kujua na wanaposikia kilio kikuu na kutii, wataokolewa.
Toafuti ya siku 75 kati ya siku 1260 na 1335 inahusika na kipindi cha kukimbilia milimani (siku 30) pamoja na kipindi cha kusubiri tangazo la marejeo ya Yesu mara ya pili (siku 45). Kipindi hiki ni sawa na miaka mitatu na nusu iliyotumiwa na wayahudi wakiwa kwenye milima ya Pella tangu mwaka 66 hadi 70 kabla ya angamizo la Yerusalemu.
Baadhi hawataweza kukimbilia milimani hivyo watakuwa wahanga na mashahidi wa kufia dini wakiwa watiifu kwa Mungu. Tunapaswa kukesha na kuomba kwa bidii ili kukuza tabia zetu zitakazotuwezesha kuwa tayari kutoa miili yetu kuwa kafara ya kumpendeza Mungu. Wapo pia watakaofungwa magerezani na wengine watakutwa na Yesu wakiwa hai gerezani na kuokolewa bila kuonja mauti kama vile Paulo na Sila walivyookolewa.

Sasa tunaweza kuweka maana ya sasa kwenye utimilifu wa unabii huu kama ifuatavyo:
“Na tangu wakati ule ambapo sadaka ya kutekezwa ya daima (Sheria ya Sabato ya Kweli) itaondolewa, na hilo chukizo la uharibifu(Sheria ya jumapili) litakaposimamishwa, itapita siku elfu na mia mbili na tisini. Heri angojaye, na kuzifikilia siku hizo elfu na mia tatu na thelathini na tano, (angojaye kwa kipindi chote cha uvumilivu mkubwa tangu siku ya tangazo la sheria ya kutokuuza na kutokununu, sheria ya vifungo na kifo, hadi kufungwa kwa mlango wa rehema).”  {Daniel 12:11,12.}

Katika kipindi kinachowakilishwa na siku 30 ikiwa ni tofauti kati ya siku 1290 na siku 1260, Wale 144,000 watakimbilia milimani wakati wa sheria ya jumapili inapotangazwa. Hawa ndiyo wanaoitwa ‘Sayuni’ na watalindwa na Mungu kama wayahudi waaminifu walivyolindwa mwaka 66 hadi 70 wakati wa angamizo la Yerusalemu.[Tazama The Great Controversy p. 426-7).
Lakini pia kuna tofauti ya siku 75 kati ya siku 1335 na siku 1260 ambapo kipindi hiki kinajumuisha vipindi viwili kwa pamoja, mosi kipindi cha siku 30 za kuanza kutoka miji mikubwa, kujiandaa na kuondoa miji midogo kwenda milimani na siku 45 zinawakilisha kipindi cha watakatifu kukaa milimani sawa na miezi 42 ya mateso wakati wa utimilifu wa unabii wa siku 2300 sehemu ya kwanza na miaka mitatu na nusu ya kuishi milimani kusubiri angamizo la Yerusalemu.

Hitimisho.
Mwanzo wa utimilifu wa unabii wa siku 2300 ni mwaka 457KK na ulifikia mwisho mwaka 1844 katika hali ya utimilifu wa siku moja kwa mwaka mmoja. Unabii wa siku 2300 umetajwa katika matukio ya siku 1260, siku 1290 na siku 1335. Mwanzo wa utimilifu wa unabii wa siku 1260 ni mwaka 538 na ulifikia mwisho wake mwaka 1798 kwa tukio la jereha la mauti baada ya Papa kukamatwa mateka na kufia ufaransa. Siku 1260 zinahusika na kipindi cha miaka 1260 ya mateso kutoka kwa kanisa la Rumi lililokuwa na mamlaka kamili ya kiserikali na kidini. Tukio kubwa katika unabii wa siku 1260 ni kuwekwa kwa sheria ya kuwaua wale waliokuwa kinyume na kanisa la Rumi. Unabii huu utajirudia wakati jeraha la mauti litakapopona kikamilifu kwa kanisa la Rumi kurejea tena kwenye mamlaka kamili ya kidini na kiserikali na kuweka sheria ya kuwaangamiza wale watakaokataa kutii sheria ya jumapili. Mwanzo wa utimilifu wa unabii wa siku 1290 ndio mwanza wa utimilifu wa unabii wa siku 1335 ambapo tukio linaloashiria mwanzo huu ni kuondolewa kwa sadaka ya kutekezwa ya daima na kusimamishwa kwa chukizo la uharibifu. Kujirudi kwa utimilifu wa unabii huu ni wakati wa tangazo la kufutilia mbali sheria ya Sabato ya kweli na mahali pake kusimamisha sheria ya jumapili. Mwanzo wa kipindi hiki ni mwaka 508 ambapo mwisho wa kipindi cha siku 1290 ni mwaka 1798 na mwisho wa kipindi cha siku 1335 ni mwaka 1843 kuelekea 1844.
Wakati chukizo la uharibifu litasimamishwa na ndani ya kanisa kutokea nje, lile kosa lifanyalo ukiwa litafanyika ndani ya kanisa asi la SDA. Hii ni kwa sababu viongozi wa kanisa asi la SDA, siyo tu kwamba hawataijali Sabato, bali pia watawalazimisha waumini wa kanisa hili kuitunza na kuiheshimu siku ya kwanza ya juma, jumapili badala ya siku ya saba ya juma Sabato. Jambo hili litasababisha ghadhabu ya Mungu na hukumu zake kuanza katika nyumba yake. Wakati hukumu za Mungu zinashuka juu ya dunia, watunza Sabato wa kweli, yaani masalio wa kanisa asi la SDA ambao waliamua kutoka na kukimbia kwa kujitenga na kanisa hilo, watasondwa kidole kuwa ndio wanaosababisha hukumu za Mungu hivyo watatafutwa ili wauwawe. [Tazama The Great Controverdy p. 635.]

“Na kama Bwana asingalikatiza siku hizo, asingeokoka mtu yeyote; lakini kwa ajili ya wateule aliowateua amezikatiza siku hizo.” Marko 13:20.

“Usiogope mambo yatakayokupata; tazama huyo ibilisi atawatupa baadhi yenu gerezani ili mjaribiwe, nanyi mtakuwa na dhiki siku kumi. Uwe mwaminifu hata kufa, nami nitakupa taji ya uzima.” Ufunuo 2:10.

Somo linalofuata ni somo la “Hema Takatifu”.

kwa mawasiliano wasiliana na 0756959525/0752164685





Share:

Maoni 17 :

  1. Enter your comment...ubarikiwe mtumishi wa Bwana

    JibuFuta
  2. Barikiwa sana jitahidi zaidi na zaidi kuchimbua magombo kwaajili ya watu wote pia.

    JibuFuta
  3. Maoni haya yameondolewa na mwandishi.

    JibuFuta
  4. Barikiwa mtumishi. Jarbu kuweka option ya kudownload kwa mfumo wa PDF itapendeza zaidi....Mungu akutie nguvu

    JibuFuta
    Majibu
    1. Kweli kabisa ili tuprint kwa ajili ya watu wengine

      Futa
  5. Barikiwa kwa kazi njema mnayoifanya

    JibuFuta
  6. Umejitahidi sana KUWADANGANYA WATU KWA KUTUMIA VIPANDEVIPANDE VYA NUKUU MBALIMBALI

    NA WATU WASIPOKIWA MAKINI KUJISOMEA WENYEWE VITABU MBALIMBALI VYA ROHO YA Unabii utadumu KUWASHIKIA AKILI

    JITAHIDI UTUBU UREJEE UACHE KAZI YA YULE MWOVU

    JibuFuta
    Majibu
    1. Sikitiko langu liko juu yako wewe unayekanusha maandiko ya Unabii wa Biblia na yale ya Nabii Ellen ukiwashutum wale wanaolihubiri neno kwa ujasiri, ushupavu na kujitoa kwamba wanapotosha. Amini nakuambia siku ya hukumu maneno yako uliomwambia mtoa somo atubu yatakua hukumu juu yako mwenyewe.

      Futa
  7. Kipindi cha Nuhu alihubiri hivi akionya watu badala yake aliitwa Mzushi, mpotoshaji, mtishaji na mwongo hatimae gharika ikaja ikawakumba bila maandalizi wakaangamia.

    Lutu kule Sodoma aliwaonya watu mpaka wakwe na mashemeji juu ya angamizo la miji ile miwili(sodoma na gomora) lakini walimshutum na kutaka hata kumfilauni yeye akakimbia akaiponya roho yake wote wakaangamia.

    Israel kabla Yesu hajaja alimtuma Yohana mbatizaji kulihubiri taifa juu ya ujio wa Yesu hawakumuamini wakamsukia njama wakamfunga na kumuua na hata Masihi akaja kwao wasimjue hata leo.

    Yesu mwenyewe aliwaonya Israel juu ya angamizo la Yerusalem hawakumsadiki na hata yeye mwenyewe akaondoka akiulaani kua ameuacha ukiwa na baadae ukaangamizwa wote kisisalie kitu ndani yake.

    Kwaio tambua kwa kila kizazi Mungu alikua anachagua watu wanyofu ili wauonye ulimwengu kabla ya dhahama yoyote ile. Nuhu, Musa kwa Misri, Eliya kwa Israel, Yona kwa Ninawi, Ezekiel, Yohana mbatizaji, taifa la Israel kwa mataifa, Yesu mwenyewe Juu ya Israel na ulimwengu, nk

    Na hata leo hii kabla ya kuja Yesu mara ya pili Mungu anawachagua watu wa kuuonya ulimwengu kabla ghadhabu ya Mungu Ufunuo 14:9-12 juu ya wanadam watakao msujudu Papa(Mnyama) na kujiunga umoja wa makanisa(Sanamu yake) na (chapa yake) kuitukuza sabato ya uongo yaani jumapili .watu hawa wanyenyekevu wataitwa Wazushi, waongo, wachonganishi, wavunja amani, waleta migogoro, wasema vibaya dini za watu, magaidi, nk kama vile alivyoiywa Nuhu majina yote mabaya. Ila mlango wa rehema utakapofungwa na mapigo kushuka ndio watu wote waliobeza watakua wamechelewa milele kama waliombeza Nuhu na wakachelewa kuingia safinani milele.
    Songa mbele mtu wa Mungu, uonye ulimwengu na Makanisa pia(Likiwemo kanisa la Mungu SDA) usiogope kama Yesu alivyosema ktk Matayo 10:14-42.

    0655660044 kwa aliependa ujumbe na akataka kujifunza zaidi anitafute na pia hata yule aliechukizwa na aitamani kuitoa roho yangu kwa nilioyanena atanitafuta.
    kwa maana bora kufa kwa kumshudia Yesu na kuuonya ulimwengu kuliko kuyapata mazuri yote ya dunia hii.

    Roho wa Mungu anene nanyi nyote.

    JibuFuta
  8. Barikiwa sana mtu wa Baba

    JibuFuta
  9. Barikiwa Sana Mjoli Nyamika

    JibuFuta
  10. Asante sana! Pia kuna mengine unge pashwa kufundisha sababu usipo ya fundisha UTADAIWA NA BWANA!
    Isupernover@gmail.com

    JibuFuta
  11. Ubarikiwe sana mtumishi wa BWANA nimesoma na kuelewa vema, BWANA atusaidie sana

    JibuFuta
  12. Nahitaji uewelewa zaidi kitabu hiki maana kinani saidia sana ktk maisha yangu kwa maendeleo ya kristo

    JibuFuta

Popular Posts

Lebo

Recent Posts

Pages